» » SABABU KUU TATU ZA KUJARIBIWA KWA MTU



Watu wengi wamekuwa wakuwa wakijihoji kama kweli mtu amezaliwa mara ya pili na bado ni mwombaji kwa nini anaingia majaribuni, kwanini Mungu ana yaruhusu majaribu?
Kujaribiwa ni kupewa mtihani ambao unatakiwa uufanya na mwamuzi wa mwisho kwamba utapata alama  0 au 100 ni wewe.

Zifuatazo ni sababu za kuachiliwa kwa majaribu kwetu:


1.  Kuongeza imani
Kama nilivyosema hapo juu kwamba majaribu ni mtihani ambao unapewa wewe uufanye na baadaye matokeo huja kama ni kushinda au kushindwa. Unaposhinda maana yake unakuwa umeongezeka kiimani na hata wakati mwingine ukikutana na jaribu la namna hiyo haliwezi kukuyumbisha kwa sababu una kumbukumbu kwamba hapo awali ulipita katika jaribu hilo na ukalishinda. Na hata ukipita katika jaribu kubwa zaidi ya lile la awali unakuwa na matumaini na imani kwamba utashinda kama ulivyoshinda katika jina la Yesu.

1 Petro 1:7 “ili kwamba kujaribiwa kwa imani yenu, ambayo ina thamani kuu kuliko dhahabu ipoteayo, ijapokuwa hiyo hujaribiwa kwa moto, kuonekane kuwa kwenye sifa na utukufu na heshima, katika kufunuliwa kwake Yesu Kristo.”

2. Kuimarisha kiroho
Unapopita katika majaribu maana yake unakuwa unafanya mazoezi ya mwili ambayo kwa wakati huo unaona kama unaumia lakini baadaye mwili huimarika na kuwa na uwezo wa kunyanyua vitu vizito, kuzuia vitu fulani au kumzuia adui. Kama ilivyo kwa mtu anayefanya mazoezi ya kutunisha misuli kwa kunyanyua vyuma vizito, misuli huvunjika na kuwa dhaifu na baadaye huimarika. Vivyo hivyo hata kwa mtu anayepitia majaribu huwa dhaifu kwa muda na baadaye huwa imara kiroho yaani kiroho chake hukomaa kiasi kwamba hakuna kitu chochote ambacho kinaweza kumyumbisha katika imani. Iwe ni ugumu wa maisha, kukosa mke, kuchelewa kuolewa, kukosa mtoto katika ndoa, kuugua kwa muda mrefu n.k

Kama misuli inavyokuwa imara baaada ya mazoezi vivyo hivyo hata imani ya mtu au kiroho cha mtu huwa imara baada ya majaribu.

Yakobo 1:2-4 “Ndugu zangu, hesabuni ya kuwa ni furaha tupu, mkiangukia katika majaribu mbalimbali; mkifahamu ya kuwa kujaribiwa kwa imani yenu huleta saburi.
 Saburi na iwe na kazi kamilifu, mpate kuwa wakamilifu na watimilifu bila kupungukiwa na neno.”

3. Ili kuwasaidia watu wengine
Wakati mwingine Mungu huyaachilia majaribu kwetu ili baadaye tuje tuwasaidie watu watakao pita katika majaribu kama tuliyoyapitia sisi. Mungu hututumia kuwafariji na kuwatia moyo wengine waliokatika jaribu kama tulilolipitia.

2 Wakorintho 1:3-5 “Na ahimidiwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa rehema, Mungu wa faraja yote; atufarijiye katika dhiki zetu zote ili nasi tupate kuwafariji wale walio katika dhiki za namna zote, kwa faraja hizo, tunazofarijiwa na Mungu. Kwa kuwa kama vile mateso ya Kristo yanavyozidi kwetu, vivyo hivyo faraja yetu inazidi kwa njia ya Kristo.”


Kukwepa kutokuwa na majaribu ni sawa na kuikwepa fursa ya kuinuliwa na Mungu.
 Yesu alitumikiwa na Malaika baada ya kumshinda Shetani na Paulo Mtume alizidi kutumiwa na Mungu kwa viwango vya juu sana kwa sababu alikuwa akikumbana na majaribu mara kwa mara na kuyashinda.

HITIMISHO: Pamoja na faida hizo tatu za majaribu lakini ni vyema pia tukatambua Mungu hawezi kutujaribu katika mabaya. Mabaya hayo ni kama wizi, uzinzi, uasherati na mengine yanayo fanana na haya yote hutokana na shetani kwa tamaa zetu wenyewe wala si Mungu.


Yakobo 1:13-14  “Mtu ajaribiwapo, asiseme, Ninajaribiwa na Mungu; maana Mungu hawezi kujaribiwa na maovu, wala yeye mwenyewe hamjaribu mtu. Lakini kila mmoja hujaribiwa na tamaa yake mwenyewe huku akivutwa na kudanganywa.”

Mithali 27:21 “……….Na mtu hujaribiwa kwa sifa zake.”

Unataka kuokoka?     Tuma ujumbe kwa WhatsApp au sms kwa namba 0625966236 ukianza na neno "NATAKA KUOKOKA"

Pakua App Ya Injili Halisi -Bofya Hapa Flower
HII NI INJILI HALISI MINISTRY, KWA MAWASILIANO +255 621 261 295

About INJILI HALISI MINISTRY

Zachary, most known as Zakacheka is the founder of the Injili Halisi Ministry. He is a member of Full Gospel Bible Fellowship Church.. He lives in Mwanza,Tanzania. 0621261295.
«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post

No comments:

Leave a Reply