» » SOMO: SIRI YA MAFANIKIO KATIKA MUNGU


Na Mchungaji Isaya, 
Katika dunia ya leo Mungu anaonekana maskini sana, ndio maana mtu akifanikiwa anaitwa majina ya kila aina; mara jambazi, freemason, mla rushwa n.k.
Tunapozungumzia mafanikio, hatuongelei magari, majumba, pesa bali neno mafanikio linatokano na neno kufanikiwa. Hivyo maana ya kufanikiwa ni kupata kitu kile ambacho kilikuwa ni haja ya moyo wako, kiwe kizuri au kibaya. Mtu aliyefanikiwa maana yake ni mtu aliyepata kitu alichokuwa akikihitaji au jambo alilolikusudia. Tunapata mafanikio kwa njia ya kidunia(kibinadamu) pia yapo mafanikio yatokanayo na Mungu mwenyewe. Mpaka upate kitu cha Mungu mwenyewe halisi si kitu rahisi rahisi.

Kila mwanadamu ana mahitaji na unapofanikiwa kuna mambo mawili hutokea:-


Jambo la kwanza Moyo huchangamka, hufurahi: Biblia inasema katika Mithali 17:22 kwamba “Moyo uliochangamka ni dawa nzuri” Kumbe moyo unapofurahi, furaha ikiingia matatizo madogo madogo katika mwili yanajifia menyewe.
Jambo la pili mwili hupata nguvu: nguvu haziko mwilini bali ziko kwenye akili. Kuna wakati mwili unaweza kuwa unaona umechoka kabisa, umelala ndani unajiona dhaifu lakini mara ukapigiwa simu ukiambiwa kuna kazi mahali fulani ya pesa nzuri tu, hapohapo akili itakuijia namna ya kufanya na mara utapata nguvu.Unapofanikiwa unapata nguvu za kuendelea kuamini kuwa Mungu anaweza kukufanikishia hata kwa hayo mengine na unapata nguvu za kusonga mbele. Unaofurahi sio mwili bali ni moyo. Ukipata nguo nzuri unavaa mwili lakini moyo ndio unafurahi. Moyo ukikasirika hata kama umevaa nguo mpya utaona ni kuukuu.
Mithali 13:12 “Kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua. Bali haja ya mtu ikipatikana, ni mti wa uzima.”

Kuna njia kuu tatu za kufanikiwa katika jambo lolote lile hapa duniani.


Njia ya kwanza ni Elimu: ni muhimu sana watu kuwa na elimu katika ulimwengu wa leo kwa sababu mambo hayawezi kufanikiwa pasipo maarifa.  Elimu inaweza kukutoa sehemu moja hadi nyingine. Kila jambo linahitaji elimu na elimu si ya shuleni tu bali elimu hupatikana popote pale ulipo; kwa mfano umemuona dada fulani kafunga kilemba chake vizuri na wewe unafunga kama yeye, watu wakikuona wanasema ‘mama fulani leo umetokelezea hatariii, hongera’ kumbe umeigilizia, ulipata elimu ya kufunga kilemba kutoka kwa dada yule.  Ukisoma Mithali 15:14  inasema “Moyo wa mwenye ufahamu hutafuta maarifa” kumbe tunapaswa kuyatafuta maarifa ili tuwe na ufahamu na tuweze kufanikiwa  kwa jambo fulani. Mtu mwenye maarifa ya jambo fulani uwezo wake wa kufanikiwa huwa ni mkubwa sana.                                             Mithali 24:5 “…mtu wa maarifa huongeza uwezo;”                    Elimu inaweza kukufanya ukaketi kwa wakuu. Danieli 1:3-6 “Mfalme akamwambia Ashpenazi, mkuu wa matowashi wake, awalete baadhi ya wana wa Israeli, wa uzao wa kifalme, na wa uzao wa kiungwana; vijana wasio na mawaa, wazuri wa uso, wajuzi wa hekima, werevu kwa sababu ya maarifa yao, wenye kufahamu elimu, watakaoweza kusimama katika jumba la mfalme; tena alimwambia awafundishe elimu ya Wakaldayo, na lugha yao.Huyo mfalme akawaagizia posho ya chakula cha mfalme, na ya divai aliyokunywa, akaagiza walishwe hivyo muda wa miaka mitatu; ili kwamba hatimaye wasimame mbele ya mfalme.”

Njia ya pili ni watu: Mungu anaweza kutumia watu ili kutufanikishia mambo yetu. Watu wanaweza kukusaidia kwa kukupa hiki au kile ili ufikie malengo yako. Inaweza ikawa ni kukusomesha, kukupa mtaji, kukutafutia kazi au hiki au kile.

Njia ya tatu ni Mkono wa Mungu mwenyewe: mkono wa Mungu unapotaka kutenda hauchagui wenye elimu au wasio na elimu. Mkono wa Mungu hauhitaji refarii wa kukupigia debe ili upate kazi au uolewe. Mkono wa Mungu mwenyewe unapotenda jambo huwa hauchanganywi na kitu chochote. Mungu ni Mungu mwenye wivu hivyo anapotaka kutenda huwa natenda mwenyewe ili zile sifa na utukufu usiwe wa kugawana kwa wanadamu na Yeye, Yeye hutaka sifa zote ziwe zake. Mkono wa Mungu mwenyewe unamtambua na kumtumia mtu yeyote yule bila kujali elimu yake. Petro na Yohana hawakuwa na elimu kubwa ya darasani lakini walichapa kazi ya Mungu na ikasonga mbele. Mkono wa Mungu unamtambua na kumtumia yeyeto yule sawa na Mungu apendavyo. Mungu akimgusa mtu aje kukuoa hautasumbuliwa katika ndoa, fahamu wanadamu wanakupa mke/mme lakini hawakusaidii kuishi naye bali Mungu anakupa mke/mme na anakupa akili ya kuishi naye. Mungu akitenda jambo  akili ya kibinadamu haitafasri.

Unaweza ukafanikiwa kwa njia ya elimu au watu lakini njia hizi huwa zina kasoro. Watu wakitusaidia kupata mafanikio watataka kurudishiwa shukurani na kama hautafanya hivyo tayari ni kosa kwa watu hao.

Mungu hafanyi kwa sababu umeomba bali  Mungu hufanya kwa sababu unatembea vizuri na Mungu, kwa sababu unauhusiano mzuri na Mungu.

Kwa Hana na Sarai njia ya elimu na watu zilishindwa kuwasaidia ili wapate watoto lakini Mkono wa Mungu mwenyewe uliwagusa wakapata watoto katika jina la Yesu. Tunamwamini Mungu asiyezuiwa na mazingira, utasa wa Hana haukumzuia Mungu kumpatia Hana mtoto, utasa na ubibi kizee wa Sara haukumzuia Mungu kumpatia Sara mtoto. Mungu akitaka kufanya jambo hazuiwi na kitu chochote.

Tufanye nini  ili tuuone mkono wa Mungu mwenyewe maishani mwetu?


Jambo la kwanza, jifunze kumtanguliza Mungu katika mambo yako yote unayotaka kuyafanya au unayoyafanya. Ukimtanguliza Mungu utakuwa tayari kumsikia anasema nini juu ya unachokifanya kama kwa Petro na Yohana; Petro na Yohana walimtanguliza Mungu ndio maana hata walipotishiwa kukamatwa hawakutanguliza sababu zao binafi kwamba ‘oooh sasa ona tunaenda kufungwa’   Matendo ya Mitume 4:19 “Petro na Yohana wakawajibu wakawaambia, Kwamba ni haki mbele za Mungu kuwasikiliza ninyi kuliko Mungu, hukumuni ninyi wenyewe”                                                                          Mtangulize Mungu wala si wanadamu, wanadamu inafikia mahali wanachoka kukusaidia lakini Mungu hachoki. Usiwe kama Esau aliyetanguliza njaa akauza uzaliwa wake wa kwanza.                    Mathayo 6:33Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.”

Jambo la pili, kubali kuanza na mambo madogo:  kubali kuanza mambo madogo yaliyo manyonge, dhaifu na baadaye Mungu atakuinua. Mungu huanza na watu waliochini kabisa wasiojua chochote na hao ndio huwatumia na baadaye huwainua na kuwapandisha juu. Je, unataka kitu kikubwa? Kubali kuanzia chini. Iwe ni kazi kubali kuanza na kazi hata ya chini kabisa na baadaye utaona unainuka; iwe ni biashara usitamani hadi uanze na mtaji mkuuuubwa, hapana! Anza na mtaji wako wa kawaida tu na Mungu atakuinua taratibu utayafikia mafanikio yako.

Jambo la tatu, kubali kuwa mvumilivu:Mungu hatubariki kwa sababu tunataka tubarikiwe bali Mungu hutubariki kwa sababu ni muda muafaka wa kubarikiwa.                                            Unamkuta binti analalamika “yaani kwa kweli muda unaenda hata siolewi, angalia matiti yanaanza kuning’inia” binti nakushauri vumilia tu,hayo matiti  yataning’inia lakini hayawezi kudondoka, kuna watu wanapenda matiti makubwa kama ya kwako.             
            
Wakati mwingine usitamani mafanikio ya mwenzako kwa sababu hujui siri ya mafanikio yake.                                                                                      

Pakua App Ya Injili Halisi -Bofya Hapa Flower
HII NI INJILI HALISI MINISTRY, KWA MAWASILIANO +255 621 261 295

About INJILI HALISI MINISTRY

Zachary, most known as Zakacheka is the founder of the Injili Halisi Ministry. He is a member of Full Gospel Bible Fellowship Church.. He lives in Mwanza,Tanzania. 0621261295.
«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post

No comments:

Leave a Reply